Lashkar-e Tayyiba (LeT), ambayo pia inajulikana kama Jeshi la Waadilifu, ni kundi la kigaidi lenye makao yake nchini Pakistani ambalo lilianzishwa miaka ya themanini. LeT imetekeleza shughuli, yakiwamo mashambulio kadha ya ngazi za juu, dhidi ya majeshi ya India na shabaha za kiraia tangu mwaka 1993. Kundi hilo pia limeshambulia Majeshi ya Muungano nchini Afuganistani. LeT ilihusika na mashambulio ya kigaidi ya mnamo mwezi Novemba, mwaka 2008 jijini Mumbai, India, yaliyowaua watu 166 – wakiwamo raia sita wa Marekani – na kuwajeruhi wengine zaidi ya 300.
Mnamo tarehe 26 mwezi Disemba, mwaka 2001, Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ya Marekani ilitaja LeT kuwa Kundi la Kigaidi la Kigeni chini ya kifungu 219 cha Sheria ya Uhamiaji na Uraia, kama ilivyorekebishwa. Hapo awali, mnamo tarehe 20 mwezi Disemba, mwaka 2001, Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ilitaja LeT kuwa Gaidi wa Kimataifa Mwenye Sifa Maalumu kuambatana na Amri ya Rais 13224, kama ilivyorekebishwa. Matokeo yake ni kwamba, mali yote na maslahi ya LeT katika mali, vyote vilivyoko chini ya mamlaka ya Marekani vimezuiwa, na watu wa Marekani kwa jumla wamekatazwa kushiriki kwenye miamala yoyote na LeT. Ni kosa la jinai kutoa kwa makusudi, au kujaribu au kula njama ya kutoa, msaada wa nyenzo au rasilimali kwa LeT.